ZINAZOVUMA:

Mkutano Mkuu Tampro wafana, Dkt Dau, Prof Assad watoa ya moyoni

Chama cha Wataalamu wa Kiislamu TAMPRO kimefanya mkutano wake mkuu...

Share na:

Chama cha Wataalamu wa Kiislamu (Tanzania Muslim Professionals Association – TAMPRO) kimefanya mkutano wake mkuu wa mwaka 2023 kwa mafanikio makubwa ambapo wanachama Zaidi ya 300 walishiriki.

Akizungumza katika mkutano huo, Makamu Mkuu wa Chuo cha Kiislam Morogoro (MUM), Prof Mussa Assad amewashauri wanachama pamoja na waislam kwa ujumla kuanzisha miradi itakayowakwamua kiuchumi.

Baadhi ya miradi ambayo ameipendekeza ni pamoja na uvuvi, kilimo na biashara huku akisisitiza kuwa sehemu kubwa ya umma wa waislam wako katika sekta hizo.

“Kwa muda mrefu watu wetu wako kwenye uvuvi, ukienda feli utakuta wanafanya shughuli zao kizamani, wanahitaji kuwezeshwa ili kuvua kisasa, eneo hilo mnaweza kufanya kitu na watu wakanufaika. Vilevile, mama lishe wanafanya kazi zao kizamani, suala la utunzanji wa fedha ni tatizo, ni jukumu la wataalam kwenda kutoa elimu”.

“Wakati nakuja nilibeba kipeperushi hiki cha Azampay, nadhani hawa wanaweza kusaidia jamii kutatua tatizo la kutunza fedha. Mfumo wao unaweza kutumika kuwawezesha mama lishe kujifunza njia nzuri za kuhifadhi fedha na hivyo kujikwamua kiuchumi”.

Aidha, Prof Assad ambaye alifika katika mkutano huo kama mgeni rasmi, amesema lazima taasisi ziwaze kuwanasua wananchi kiuchumi.

“Kwa mfano kule Morogoro, kuna spices nzuri sana, mfano karafuu, Vanila, na nyinginezo, tatizo kubwa walilo nalo ni la ukaushaji na ufungaji wa bidhaa.

Tampro mnaweza kuingia na kutoa mashine za kukaushia, pamoja na vifungashio kisha bidhaa hizo zikawekwa nembo Tampro na kuziuza, mtakuwa mmesaidia sana watu.

Katika hatua nyingi Prof. Mussa Assad ambaye kitaalamu ni MKaguzi wa hesabu, ameipongeza TAMPRO – SACCOS kwa kufanikiwa kutoa mikopo kwa wanachama wake huku akiwataka kuongeza jitihada ya kuwafikia wanachama wengi Zaidi.

Prof Assad amesema anaitazama Tampro Saccos kama chombo cha mfano kwa umma wa kiislam hapa nchini kwani zipo nyingi za Kiislam ambazo zilijaribu kuifanya kazi hiyo lakini hawakufika mbali.

“Ni SACCOS ya muda mrefu sana na imestahimili, nimesikia fedha ambazo zimetolewa kuwakopesha wanachama, ni hatua kubwa sana ila bado jitihada zaidi zinahitajika ili kuwafikia wengi zaidi,” alisema Prof. Assad.

Amesema kutoa Kiasi cha Bilioni 10 kama mkopo katika kipindi cha miaka Zaidi ya 10 ni mafanikio makubwa, lakini bado haitoshi.

Naye, Balozi Mstaafu Dkt Ramadhani Kitwana Dau ameungana na Prof Assad kuzishauri Taasisi mbalimbali za Kiislam kuanza kuwekeza kama kweli zinataka kujikwamua kiuchumi.

Dkt Dau ambaye alifika katika mkutano huo kama mgeni Maalum, amesema kwa karne ya sasa ni vizuri taasisi zikawaza kuwekeza katika sekta mbalimbali ili kujikomboa kiuchumi.

“Miongoni mwa mambo ambayo yanakwamisha maendeleo ya Taasisi nyingi hapa nchini, ni kukosa uwezo wa Kiuchumi, nashauri Taasisi za kidini ikiwemo Tampro zitafute namna ya kuanzisha vitega uchumi, na watafute watendaji ambao watabuni miradi na kuisimamia vizuri,” alisema Dkt Dau.

“Tufanye uwekezaji, tuajiri watalaamu wa kusimamia mipango yote ya Kiuchumi ili Taasisi zijiendeshe, tunaweza kufanikiwa zaidi kwenye hilo iwapo tutajipanga vizuri,” aliongeza Dkt. Dau.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taasisi ya TAMPRO Haji Mrisho amesema amefurahishwa na mahudhurio ya mkutano huo huku akisisitiza kuwa mkutano huo umefana kwa asilimia 100. Amewapongeza waislam waliojitoa kwa hali na mali ili kufanikisha mkutano huo na amewatia moyo kuwa jambo wanalolifanya linafaida kubwa kwa vizazi vya sasa na hapo baadae.

“Tumefurahi kuona viongozi wetu, Prof Mussa Assad na Mwenzake Balozi Mstaafu Dkt Ramadhani Dau wameungana nasi, hawa ni watu ambao muda wote wapo tayari kuchangamana na waislam wenzao tunawapongeza sana kwa moyo wao,” alisema.

Aidha akieleza kuhusu mafanikio ya TAMPRO Saccos, bosi huyo wa chama cha wataalam wa kiislam amesema Tampro Saccos imefanikiwa kutoa mikopo inayogharimu Shilingi Bilioni 13 kwa wanachama wake kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2010 hadi 2024.

Amesema lengo la Tampro ambayo ilianzishwa mwaka 1997, ni kuwawezesha Waislamu na Jamii kwa ujumla ili kuboresha maisha yao katika nyanja mbalimbali za Kimaisha.

Vilevile amesema pamoja na kutoa mikop hiyo, bado wanaendelea kutafuta njia za kuhakikisha wanaiwezesha zaidi jamii Kiuchumi ikiwemo kutumia ushauri wa wataalam wa kuanzisha miradi ya maendeleo.

“Tumefanikiwa kutoa mikopo kwa wanachama wetu kupitia TAMPRO SACCOS na bado tunaendelea kutafuta mbinu mbalimbali za kuwawezesha wanachama wengi zaidi,” alisema Mrisho.

Amesema Mkutano umejadili changamoto za ajira na kutafuta mbinu za kukabiliana na jambo hilo, kutafuta uwezo wa kuwasaidia Kiuchumi vijana na akinamama, na pia umejadili namna ya kuijengea uwezo Taasisi hiyo na kuonekana ni vema kuanzisha miradi ya maendeleo.

“Hivi sasa mbali na Serikali, sekta binafsi nayo inatoa ajira, kwa hiyo tumejadili namna ya kutengeneza fursa za ajira na kutafuta njia za kuwawezesha wafanyabiashara wadogo wakuze biashara zao, vile vile tumejadili namna ya kuiongezea Taasisi yetu nguvu ya Kiuchumi,” alisema.

Endelea Kusoma

Anguko la mfumo wa Crowdstrike umesababisha kapuni nyingi duniani kushindwa kutoa huduma

Chaguo la Mhariri

Habari Mpya