Mwenyekiti wa Wafanyabiashara Kariakoo, Martin Mbwana amesema mgomo unaoendelea leo unasababishwa na kikundi cha watu wachache wenye maslahi yao binafsi huku akiomba wachukuliwe hatua na kuahidi kutoa ushirikiano kwa vyombo vya usalama.
Ameyasema hayo leo Jumanne Mei 16, 2023 kufuatia baadhi ya maduka kuendelea kufungwa, licha ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa jana kuwataka wafanyabiashara hao kusitisha mgomo huku akiahidi kushughulikia kero zao kikao cha kesho Jumatano ya Mei 17, 2023.
Mbwana amesema kilio chao kama wafanyabiashara ilikuwa ni kusikilizwa na Rais Samia Suluhu Hassan, na katika kuonyesha kuwa amewasikia alimtuma Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
“Alipokuja aliwaomba wafanyabiashara wafungue maduka na kuahidi kuwasiliza siku ya Jumatano. Nashangaa wafanyabiashara kuwa hawana imani na Waziri Mkuu,” amesema
Amesema shida ni kikundi cha watu wachache wanaoonekana kuwa na manufaa na mgomo huo huku akieleza kuwa ameomba msaada kwa vyombo vya usalama kuwachukulia hatua na kusema yupo tayari kutoa ushirikiano.
