Serikali ya Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo inawashutumu wanajeshi wa Rwanda kwa kuvuka mpaka na kuingia katika ardhi yake.
Jeshi la Congo lilitoa taarifa kuelezea madai ya uvamizi katika jimbo la Kivu Kaskazini na kuuita kuwa ni uchokozi usiovumilika.
Rwanda haijatoa tamko lolote kuhusiana na tuhuma hizo, lakini mara kwa mara imekuwa ikikana tuhuma za uvamizi wowote ndani ya ardhi ya ‘DRC’.
Awali Rwanda ilikanusha shutuma za serikali ya DRC kwamba inaunga mkono kundi la waasi linalojulikana kwa jina la M23, ambalo limefanya mashambulizi mengi mashariki mwa nchi hiyo.