Serikali ya Kenya na chama pinzani nchini humo cha Azimio wanatarajiwa kuanza mazungumzo yanayolenga kutafuta muafaka baada ya maandamano ya vurugu za kupinga uchaguzi uliopita pamoja na kupanda kwa gharama ya maisha.
Mazungumzo hayo yataratibiwa na Rais wa zamani wa Nigeria, Olusegun Obasanjo ambapo yanatarajiwa kutoa suluhu ya mvutano unaoendelea kati ya kiongozi wa upinzani Raila Odinga na Serikali.
Muungano wa upinzani wa Azimio uliongoza maandamano mwezi Machi na Julai dhidi ya utawala wa Rais William Ruto kupinga kupanda kwa gharama ya maisha na kutaka mageuzi katika tume ya uchaguzi kwenye Taifa hilo.
Maandamano hayo yalionekana kuzidi baada ya serikali kutangaza kuongezwa kwa ushuru katika baadhi ya bidhaa kwa kile Rais Ruto alisema hatua hiyo inalenga kuimarisha maendeleo nchini mwake.